Tuesday, 15 May 2018

Watu 52 wafariki Marekani ikifungua ubalozi mpya Jerusalem



Raia 52 wa Palestina wameuawa na wengine 2,400 wamejeruhiwa na wanajeshi wa Israeli katika mapigano mabaya kuwahi kushuhudiwa tangu mwaka 2014 katika mpaka wa Gaza, maafisa wa Palestina wanasema.

Raia wa Palestina wamekuwa wakiandamana kwa wiki kadhaa lakini zimechacha leo wakati ubalozi mpya wa Marekani umefunguliwa mjini Jerusalem hatua iliyowaghadhabisha Wapalestina.

Wanaitazama hatua hiyo kama Marekani kuunga mkono utawala wa Israel katika mji huo mzima wakati wapalestina wanadai haki ya umiliki wa eneo la mashariki mwa mji huo.

Maafisa wa vyeo vya juu kutoka Marekani watahudhuria sherehe hiyo leo akiwemo binti ya Rais wa Marekani Donald Trump Ivanka na mumewe Jared Kushner.

Wengi wa maafisa kutoka Muungano wa Ulaya hawatahudhuria.

Uamuzi wa Trump wa kuhamisha ubalozi huo kutoka Tel Aviv umegadhabisha Wapalestina ambao wanadai eneo la Jerusalem Mashariki ni mji wao mku wa badaye.

Israel ilichukua udhibiti wa eneo la Jurusalem mashariki mwaka 1967 wakati wa vita vya Mashariki ya kati, na inautaja mji huo kuwa wake na usiogawanywa.




Hatua hiyo ya Trump ya mwaka uliopita ya kuutambua mji wa Jerusalem kuwa mji mkuu wa Israel ilivunja msimamo wa wastani wa Marekani kwa suala la mji huo na kwenda kinyume na misimamo ya nchi zingine duniani.


Ubalozi wao mdogo ulianza kutoa huduma kuanzia jana Jumatatu kwenye jengo la ofisi za ubalozi mjini Jerusalem.

Eneo lingine kubwa litatafutwa baadaye wakati ubalozi wote utahama kutoka mji wa Tel Aviv.

Sherehe za ufunguzi zilifanywa mapema ili ziweze kuenda sambamba na sherehe za miaka 70 za kuanzishwa taifa la Israel.

Rais Trump anatarajiwa kuhutubia wale ambao watahudhuria sherehe hiyo kwa njia ya video.



Kando na Ivanka Trump na Jared Kushner ambao wote ni washauri wakuu kwenye Ikulu ya White House, Waziri wa fedha wa Marekani Steven Mnuchin na naibu waziri wa mashauri ya nchi za kigeni John Sullivan watakuwa kwenye sherehe hiyo.

Muungano wa Ulaya umepinga vikali kuhamishwa kwa ubalozi huo na mabalozi wengine wa nchi za EU hawatahudhuria sherehe hiyo.

Hata hivyo wanadiplomasia kadhaa wa kigeni wanatarajiwa kuhudhuria wakiwemo waakilishi kutoka Hungary, Romania na Jamhuri ya Czech ambayo ilizuia taarifa ya pamoja ya EU kuhusu suala hilo.

Marais wa Guatemala na Paraguay pia nao wanatarajiwa kuhudhuria; nchi hizo zote mbili ziliamua kuhamisha balozi zao kwenda Jerusalem baada ya Trump kutoa tangazo hilo.



Waziri mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu alitoa wito kwa nchi zote kujiunga na Marekani na kuhamisha balozi zao kwenda Jerusalem.

Rais wa Mamlaka ya Palestina Mahmoud Abbas ameutaja uamuzi wa Trump kama dafrao ya karne.


Maelfu ya Wapalestina wanakusanyika kuandamana kwenye ua unaotenganisha Israel na ukanda wa Gaza.

Muda wa kuhamishwa ubalozi huo umezua wasi wasi wa kuongezeka msukosuko huko Gaza


Tangu mwisho wa mwezi Machi zaidi ya wapalestina 40 wameuawa na wanajeshi wa Israel wakati wa maandamano ya mpakani.

Mkuu wa shurika la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa ameilaumu Israel kwa kutumia nguvu nyingi.

Hali ya mji wa Jerusalem ndiyo chanzo cha mzozo kati ya Israel na Palestina.

Tangu mwaka 1967 Israel ilijenga makao mengine kwa karibu wayahudi 200,000 huko Jerusalem mashariki. Makao hayo yanatajwa kuwa haramu chini ya sheria ya kimataifa, licha ya Israel kupinga hilo.

Labels:

0 Comments:

Post a Comment

Subscribe to Post Comments [Atom]

<< Home